Jux: Vanessa wa nini, sitaki shobo nishamblock

Muktasari:

Jux na Vanessa waliishi kwenye dunia moja ya mahaba kwa takribani miaka miwili kabla ya baadae kuachana ambapo Vee Money aliibukia kwenye penzi la Rotimi huku Jux akiangukia penzi la mrembo wa Kithailand anayefaamika kwa jina la Nnayika ambae kwa sasa wameachana pia

Wakati huba la msanii wa Bongofleva Vanessa Mdee na mpenzi wake muigizaji wa Marekani Rotimi likiendelea kunoga, mpenzi wa zamani wa Vanessa, msanii Jux amebuka na kauli ya 'Vanessa wa nini, sitaki shobo, nishamblock'.

Kauli ya msanii huyo mmliki nyimbo kali kama vile Sugua na Regina imekuja kwa mtindo wa ushairi kupitia wimbo mpya wa Lala wa msanii Rayvanny aliomshirikisha Jux.

Ishu iko hivi, jana Februari 1 msanii Rayanny ameachia albamu yake yenye nyimbo 23 inayoitwa Sound from Africa. Sasa wimbo namba 16 katika albamu hiyo, Rayvanny amemshirikisha Jux.

Katika wimbo huo Jux ambaye jina lake halisi ni Juma Mkambala ameimba ubeti wa kwanza na kwenye sekude ya 47 ya wimbo huo mistari anayoimba Jux inasikika kama ifuatavyo;

Ngozi laini, mtoto soap soap,
Tumbo la kuvalia crop top,
Vanessa wa nini, we dont talk talk,
Sitaki shobo nishamblock block,

Mistari hiyo imeibua hisia za kwamba huenda Jux alipotaja jina la Vanessa alikuwa akimaanisha mpenzi wake wa zamani Vanessa Mdee.

Jux na Vanessa waliishi kwenye dunia moja ya mahaba kwa takribani miaka miwili kabla ya baadae kuachana ambapo Vee Money aliibukia kwenye penzi la Rotimi huku Jux akiangukia penzi la mrembo wa Kithailand anayefaamika kwa jina la Nnayika ambae kwa sasa wameachana pia.