Hee! Nandy kuvishwa pete nyingine

HATA kama hutaki, lakini habari ndio hiyo, staa wa ngoma iitwayo Ninogeshe, Faustina Charles ‘Nandy’, anatarajiwa kuvishwa tena pete ya uchumba kwa mara ya pili.

Ndio, Nandy mwenyewe amefichua jambo hilo katika mahojiano na Vibe Weekend lililotaka kujua juu ya taarifa hizo za kuvishwa pete kwa mara nyingine wakati alishavishwa awali na mchumba wake, Billnass, Aprili mwaka jana katika shoo ya Homa.

Akizungumzia hilo, Nandy alisema pete ile ya awali iliibwa na vibaka akiwa kwenye shoo mjini Tanga, mwaka jana ndio maana analazimika kuvishwa nyingine, ila na Billnass huyohuyo.

Nandy alifafanua pia kuwa kuvalishwa pete hiyo nyingine kwa sasa hana uhakika sana, kwani hata uvalishwaji wa pete ya kwanza wazazi wake hawakuibariki.

“Wakati navalishwa pete siku ile mliona hakukuwa na wazazi wala ndugu zangu na hata wazazi, pia jambo lile halikuwapendeza wala kuliafiki,” alisema Nandy.

“Hata hivyo, kama sio kupotea kwa pete hiyo niliyovishwa, bado Billnass atapaswa kunivalisha pete nyingine mbele ya wazazi wangu.”

Kuhusu ni lini hasa atavalishwa pete hiyo, alisema hajui na jambo hilo amuachia Billnass kwa kuwa yeye ni mwanaume, na ndiye mwenye kupanga zaidi hilo kwa mila na desturi za Kiafrika.