Esma: Sitaki tena ndoa

MJASIRIAMALI na dada wa msanii wa Bongo Fleva nchini, Nasib Abdul ‘Diamond’, Esma Khan, amesema hana mpango wa kufunga ndoa tena kwa sababu aliyoyapitia ni mengi, hivyo anahitaji kuwa peke yake na uhuru ili afanye mambo yake na si vinginevyo.

Esma alisema kwa kipindi hiki ambacho yupo pekee yake amekuwa huru na anafanya biashara zake vizuri hata akifunga saa 5 usiku, hakuna wa kumuuliza tofauti na alivyokuwa ndani ya ndoa.

“Kwa kipindi hiki naona ni bora kuwa pekee yangu sihitaji ndoa na mtu yoyote kama unavyojua nina mambo mengi ya kufanya nina biashara yangu kwa hiyo muda mwingine huwa nakuwa nafuatilia mizigo kuhakikisha inafika salama.

“Na kuna muda nakuwa na wateja wengi dukani huwa nafunga usiku sana, hivyo najikuta nipo huru kwani sina mtu wa kuniuliza kwa nini ninachelewa kurudi nyumbani hiyo inanifanya nifanye biashara yangu kwa uhuru zaidi tofauti ukiwa kwenye ndoa unakuwa hauna tofauti na mtumwa kabisa, kwa sasa nipo bize na biashara zangu tu na si kingine,” alisema Esma.

Esma ambaye ni mama watoto wawili, alifunga ndoa na mfanyabishara maarufu Msizwa lakini ndoa yake ilidumu kwa miezi mitano na kuvunjika huku kila mmoja akimtoa sababu mbalimbali za kuvunjika kwa hiyo.

Hii ilikuwa ni ndoa yake ya pili kuvunjika kwani awali alifunga ndoa na Petit Man ambayo pia ilivunjika.