Diamond ashinda tuzo Marekani, Harmonize akosa

Diamond ashinda tuzo Marekani, Harmonize akosa

Muktasari:

  • Supastaa wa Bongofleva kutoka lebo WCB, Diamond Platnumz ameibuka mshindi katika tuzo za 15, The Headies za Nigeria ambazo zimetolewa usiku wa kuamkia leo Jumatatu Septemba 5, 2022 Georgia nchini Marekani.

Supastaa wa Bongofleva kutoka lebo WCB, Diamond Platnumz ameibuka mshindi katika tuzo za 15, The Headies za Nigeria ambazo zimetolewa usiku wa kuamkia leo Jumatatu Septemba 5, 2022 Georgia nchini Marekani.
Diamond ameshinda katika kipengele cha msanii bora Afrika Mashariki baada ya kuwabwaga Harmonize, Zuchu, Meddy (Rwanda), Eddy Kenzo (Uganda) na Nikita Kering (Kenya).
Hata hivyo, Diamond ameshindwa kufua dafu kwenye kipengle cha msanii bora wa Mwaka Afrika ambacho alikuwa anawania na Black Coffee, Davido, Soolking, Aya Nakamura, Wizkid na Burna Boy ambaye ameibuka mshindi.
Msanii wa Nigeria, Wizkid ndiye ameondoka na tuzo nyingi zaidi akishinda vipengele vya wimbo bora wa R&B (Essence ft. Tems), wimbo bora wa kushirikiana (Essence ft. Tems), wimbo bora wa mwaka (Essence ft. Tems), albamu bora ya mwaka (Made In Lagos)  na albamu bora ya Afrobeats (Made In Lagos).
Wasanii wengine waliofanya vizuri ni Burna Boy akishinda tuzo mbili, Davido tuzo mbili, huku Tems, Innoss'B, FireBoy DML, Patoranking, Mr. Flavour, Fave, Latifa, D'Banj na wengineo wakishinda tuzo moja moja.