Alichokisema Diamond kuhusu uteuzi wa Msemaji wa Serikali

Muktasari:

Ikiwa imepita siku moja tangu Rais Samia Suluhu Hassan kuteua makatibu wakuu, naibu makatibu wakuu wa wizara na wakuu wa taasisi mbalimbali, ambapo Grayson Msigwa akiteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali, Msanii Diamond Platnumza, amemzungumzia msemaji huyo.

Ikiwa imepita siku moja tangu Rais Samia Suluhu Hassan kuteua makatibu wakuu, naibu makatibu wakuu wa wizara na wakuu wa taasisi mbalimbali, ambapo Grayson Msigwa akiteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali, Msanii Diamond Platnumza, amemzungumzia msemaji huyo.

Diamond ameyaandika hayo leo Jumanne Aprili 6, 2021 katika ukurasa wake wa Instagram.

 Mkali huyo wa kibao cha Waah! Ameandika; “Kwa kipekee sana naomba leo niyasema machache haya: Naamini si wengi wamebahatika kukufahamu sana , ila wewe bro una roho ya kipekee sana...licha ya majukumu yako ya Ukurugenzi wa mawasiliano , ila toka nikufahamu siku zote umekua ni kiungo mzuri sana wa kusimamia mahusiano kati  ya serikali na wananchi.

“Haubagui mkubwa wala mdogo, mwenye hadhi au asiye na hadhi, mara zote panapo na jambo umekuwa ukihakikisha wote wanapata huduma sawa inapohitajika.... hauna majivuno, hauringi, ata iwe usiku wa saa tisa mara zote umekuwa ukiwapa wote huduma inapohitajika,”ameandika Diamond.

Msanii huyo ameongeza kuwa “Wengi wakipataga nafasi wanajifanyaga Miungu watu, wanatudharau na kutunyanyasa, lakini toka nibahatike kukufahamu sijawahi kuona ukibadilika kitabia, na naamini sio mimi tu ila umekuwa mtu wa watu kwa wote, na ndio maana licha ya teuzi nyingi zimefanyika ila teuzi yako imeandikwa na vyombo vingi na imepostiwa na watu wengi sana kwasababu ya uzuri wa Roho yako.

“Nimeona nikupatie sifa zako ukiwa hai na nikiwa hai...nakutakia kila la kheri, katika majukumu yako mapya ya kumsaidia Mama yetu, Rais wetu Samia Suluhu, katika Ukurugenzi wa Idara ya Habari, Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali.