Wolper: Mi’ kuhamia Tandika inawahusu?

Muktasari:

Nyota huyo wa filamu nchini, ambaye kwa sasa anakiwasha katika tamthilia inayobamba ya ‘Kapuni’ inayorushwa na DStv, akiigiza kwa jila la ‘Prisca’ a.k.a ‘Pulisika’, amesema maneno ya kukatisha tamaa yamekuwa yakiwafanya wanadamu wengi kufa masikini kwa kuamini wanachoambiwa kwamba hawataweza kufikia malengo yao.

MWIGIZAJI na mbunifu wa mavazi, Jacqueline Wolper amesema ni kweli amehamisha duka lake kutoka Kinondoni na kulihamishia Tandika na anashangazwa na wanaomsema vibaya kwa jambo hilo ambalo hawafahamu lengo lake.

Wolper amedaiwa kuwa amefulia kiasi cha kushindwa kuendelea kulipa kodi katika eneo ghali la Kinondoni na kuhamishia ofisi yake ya ushonaji eneo la bei poa Tandika.
“Ona kama hizi habari ninazoambiwa kuwa nimefulia hadi nimekimbia kulipa kodi Kinondoni na kwenda Tandika kwenye bei rahisi, uzuri wake mimi huwa siogopi maneno ya watu na napenda kile ninachofanya kutokana na uamuzi wangu, hivyo nifulie nisifulie ni mimi na hawawezi kunikatisha tamaa.
“Sana sana nawaona ni wakuja leo mjini, hivi wanapajua vizuri Tandika kwa biashara? Basi mimi nimefuata pesa kule, tena watu wa kule ni wanunuzi wazuri sana na wanapenda kuvaa,” alisema Wolper.

Nyota huyo wa filamu nchini, ambaye kwa sasa anakiwasha katika tamthilia inayobamba ya ‘Kapuni’ inayorushwa na DStv, akiigiza kwa jila la ‘Prisca’ a.k.a ‘Pulisika’, amesema maneno ya kukatisha tamaa yamekuwa yakiwafanya wanadamu wengi kufa masikini kwa kuamini wanachoambiwa kwamba hawataweza kufikia malengo yao.

Akipiga stori na Mwanaspoti, Wolper amesema yeye ni komando na ameshayazoea maneno hayo ambayo alikumbana nayo tangu alipokuwa na ndoto ya kuanza masuala ya ufundi cherehani.

Amesema alipojaribu kuwashirikisha baadhi ya watu kwenye mipango yake, wengi

walimkatisha tamaa wakimwambia hataweza huku wakimtolea mifano ya watu wengi walioanzisha biashara hiyo na kushindwa. Lakini anasema kwa kuwa yeye ni mpambanaji aliamua kuifuata ndoto yake na kuanzisha hivyohivyo na akafanikiwa hadi sasa.

“Sidhani kama Mungu aliumba watu wawe wanawakatisha tamaa wengine, hii ni tabia ambayo inakuwa kutokana na mtu anavyojiweka. Nilishawahi kukatishwa tamaa na kuambiwa kwamba sitaweza, ila mwisho wa yote nikaamini kwamba nitashinda, nikafanya na kweli nikashinda.”