Steve amuangukia Dimpoz

Muktasari:

  • Pamoja na kujitetea, Steve alipohojiwa na vyombo mbalimbali vya habari, aliomba msamaha kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wake wa Instagram.

SIKU chache baada ya kuwa gumzo kutokana na video inayomuonyesha mchekeshaji na muigizaji sauti za watu mashuhuri nchini, Steve Nyerere akinukuliwa akisema mwimbaji Ommy Dimpoz asingeweza kuimba tena, msanii huyo ameamua kumuangukia akiomba radhi.

Katika video hiyo, Steve alikuwa akihojiwa na kudai ingekuwa ngumu kwa Dimpoz kuimba tena baada ya kufanyiwa upasuaji wa koo.

Baada ya kuandamwa, Steve aliamua kuomba radhi kwa Dimpoz kwa kauli hiyo kwa bahati staa huyo wa muziki wa kizazi kipya aliamua kumkubalia, huku akimtaka asimfikirie vibaya kwa kuendelea kutuma vichekesho vinavyoelezea kauli yake hiyo vilivyochezwa na Joti na Dullvani.

Baada ya video hiyo kusambaa, Ommy Dimpoz alionekana hadharani tangu atoke kupata matibabu nchini Ujerumani akiambatana na wimbo wake mpya wa Ni Wewe’.

Baadhi ya watu katika mitandao ya kijamii walionekana kumshambulia Steve kutokana na kauli yake hiyo hususani pale alipokuwa mmoja wa watu waliotuma video ya wimbo huo katika ukurasa wake.

Pamoja na kujitetea, Steve alipohojiwa na vyombo mbalimbali vya habari, aliomba msamaha kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wake wa Instagram.

Katika ukurasa huo aliandika..’ Kwanza nichukue fursa hii kumshukuru MwenyeziMungu, lakini pili nichukue fursa hii kumuomba radhi ndugu yangu Dimpoz kwa namna alivyopokea kauli yangu niliyoitoa dhidi yake.Na zaidi niwaombe radhi Watanzania.”