Mzee Yussuf: Msinihurumie kurudi kwenye muziki

Muktasari:

Mzee Yusufu amefunguka kwa mara ya kwanza tangu atangaze kurudi kwenye muziki na kuwasihi watu wasimuhurumie

Siku moja baada ya Mzee Yussuf kutungaza kurudi kwenye muziko, amewashukia wanaomnanga na kueleza anapaswa kujihurumia kurudi kwenye muziki ni yeye na sio mtu mwingine.

Mzee Yussuf ameyasema hayo leo Alhamisi Julai 23, 2020 alikuwa akihojiwa na kituo cha redio Wasafi.

Msanii huyo alitangaza kuacha kuimba taarabu mwaka 2016 na kujikita katika shughuli za ualimu wa dini.

Hata hivyo Machi 12 mwaka huu Mzee Yussuf aliwashtua wengi pale alipoandika kwenye ukurasa wake wa Instagram kuwa anarudi mjini na ataimba mpaka agalegale.

Pamoja na kuhojiwa mara kwa mara kuhusu kauli hiyo hakuwahi kusema kuwa anarudi kwa staili gani hadi Jana Julai 22, 2020 alipoweka tangazo kwenye ukurasa wake wa Instagram na kueleza tukio la uwepo wake katika viwanja vya Dar Live sikukuu ya IDD El Haji, tukio aliloliita 'Mzee Yussuf anarudi Mjini'.

Baadhi ya watu wamekuwa na maoni tofauti, wengine wakimtukana huku wengine wakionyesha kumuhurumia kwa hatua hiyo ukizingatia alishaenda hadi kuhiji Makka.

Akihojiwa kituo cha redio cha Wasafi, Mzee Yussuf amesema watu hawapaswi kumuhurumia, kwani anatakiwa kujihurumia mwenyewe.

"Naomba watu wasiwe na jazba kuhusu maamuzi yangu, kwani kama ni kuadhibiwa nitaadhibiwa mimi”

"Isitoshe katika maamuzi haya sio kwamba nimeacha dini yangu bali nimerudi kwenye muziki hivyo waliokasirika huenda wakaja kufurahi nami siku zijazo,"amesema Mzee Yussuf.

Wakati kuhusu sababu ya yeye kuamua kurudi hakutaka kuiweka wazi na kueleza anayotaka kujua hayo atamueleza kwa ujumbe wa meseji.