Morrison ? Hadi Dorah kaamua kuweka mkeka

Muktasari:

Dorah alisema mbali na wachezaji ambao wanaunda kikosi cha Yanga kwa sasa, zamani alikuwa anampenda mshambuliaji wa kimataifa Amissi Tambwe kutokana na namna alivyokuwa anazifumania nyavu.

MSANII wa tamthilia ya kapuni, Wansukura Zacheal alimarufu kama Dorah, amemtaja winga wa Yanga, Benard Morrison kwamba ndiye atakayeiliza Simba, katika mechi ya watani itakayopigwa Machi 8.

Dorah ni shabiki wa Yanga lialia alisema Morrison ni mchezaji mwenye akili kubwa ya soka hivyo anaamini kwa beki ya Simba atawafurahisha na kuwafanya watani wao kulala mapema.

Alisema anapenda namna ambavyo Morrison anajituma mpaka dakika ya mwisho kuonyesha nia yakuisaidia timu na kwamba sare walizokuwa wanazipata kwa mfululizo ni moja ya matokeo yakuwafanya wawe imara zaidi.

“Naamini timu yangu ya Yanga itaibuka na ushindi kwenye mechi na Simba, ukiachana na Morrison kuna kina Haruna Niyonzima, Mapinduzi Balama na wengine ambao wataibeba timu siku hiyo kwa uwezo wao,”

Aliongeza kuwa “Kuna utani wa upande wa pili kutuambia sare zimezidi, binafsi naamini kwamba itafika zamu ya Yanga kucheka, Simba kabla yakuchukua ubingwa mfululizo mara mbili ilikuwa inalia lia timu yangu ndio ilikuwa inachukua mataji hayo,”alisema.

Dorah alisema mbali na wachezaji ambao wanaunda kikosi cha Yanga kwa sasa, zamani alikuwa anampenda mshambuliaji wa kimataifa Amissi Tambwe kutokana na namna alivyokuwa anazifumania nyavu.

“Tambwe alikuwa anawawezea sana Simba ni mchezaji ambae nilikuwa nafurahia nikimuona uwanjani, ila kwa sasa ni hao niliowataja, wanajituma na juhudi zao zinaonekana,” Alisema.