Mapenzi yawavuta pamoja Nyoshi, Patcho

Muktasari:

Watunzi na waimbaji hao wa zamani wa FM Academy 'Wazee wa Ngwasuma' kwa muda mrefu watengane hawakuwahi kuimba pamoja

NGOMA mpya iitwayo Mapenzi Yanauma Remix ambayo inatarajiwa kuzinduliwa kesho Julai 24, 2020  jijini Arusha kwenye shoo iliyoandaliwa na Mjengoni Classic Band, imewakutanisha pamoja wakali wa muziki wa dansi wenye asili ya DR Congo, Nyoshi El Saadat na Patcho Mwamba.

Watunzi na waimbaji hao wa zamani wa FM Academy 'Wazee wa Ngwasuma' kwa muda mrefu watengane hawakuwahi kuimba pamoja na wala kuwa na ukaribu kwa kilichoelezwa bifu lililokuwa, lakini kupitia ngoma hiyo mpya mmoja ya wanamuziki wa Mjengoni.

Wimbo huo unatarajiwa kuzinduliwa kesho Ijumaa jijini Arusha ambao wanamuziki hao wakali, yaani Nyoshi na Patcho nao watashiriki kunogesha uzinduzi huo utakaofanyika  kwenye ukumbi wa Cocorico, uliopo eneo la Kijenge.

Mbali na Patcho na Nyoshi wimbo huo umeimbwa pia na mkongwe King Kiki, Dully Sykes na  Robert Mukongya  'Digital Tiger' ambaye ndiye Rais wa  Mjengoni Classic na mtunzi wa wimbo huo.

Akizungumza na Mwanaspoti, Tiger, amesema wimbo huo unatokana na ule alioutunga ndani ya bendi yao ya Mjengoni na aliamua kuufanyia Remix kwa kuwashirikisha wanamuziki wa nje ya kundi lao  kutokana na ndoto yake ya muda mrefu ya kufanya kazi nao.

Pia amaeema alikuwa akitaka kuwakutanisha kwa kuimba pamoja kwa wanamuziki hao wakali nchini kutokana na ukweli ni muda mrefu mashabiki zao hawajapata kuwasikia wakiimba kwa pamoja tangu walipoachana walipokuwa Wazee wa Ngwasuma.

"Nashukuru nimefanikiwa kufanikisha lengo la kuwakutanisha wakali hao sambamba na King Kiki, Dully Sykes na Ijumaa tunaenda kuzindua wimbo huo katika moja ya shoo ambao inatarajiwa kuwapa raha mashabiki wa muziki wa dansi, jijini Arusha," amesema Tiger.

Aidha Tiger ameongeza kuwa watu wanajiuliza aliwezaje kuwashawishi Patcho na Nyoshi kuimba kwa pamoja kitu ambacho asilimia kubwa ya watu wanafahamu waimbaji hao wana bifu kwa kusema;

"Ukweli sikupata tabu  ya kuwakutanisha na nimegundua watu hawa hawana bifu kabisa. Ni watu wanaoongea vizuri na kusikilizana kwa kila jambo,  hivyo  ili watu waje kudhihirisha hili naloongea kama ni la kweli watafute tu kiingilio na kuja Cocorico Club kushuhudia maneno yangu," amesema mtunzi na mwimbaji huyo wa Mjengoni.