Kwa vichwa hivi, Konde Boy kalamba dume

SIKU chache zililopita Harmonize a.k.a Konde Boy alitangaza kumsaini Country Boy pamoja na waimbaji Cheed na Killy kwenye genge lake liitwalo Konde Gang.

Usajili huo unamfanya Konde Boy kuwa bosi wa vichwa vitano chini ya genge lake la Konde Gang kwani tayari alishakuwa na bwa’mdogo Ibraa na Young Skales kutoka Nigeria.

Jambo hilo limemfanya mkali huyo kulamba dume, kwani Young Skales amefanya makubwa huko, mbali na mchanaji Country Boy ni moja ya ushindi wa biashara yake ya muziki. Hii ni kutokana na ukubwa wa Country Boy kwenye muziki wa Bongo hususan michano.

Country Boy ndiye mchanaji anayesikilizwa na kushawishi vijana kufanya muziki kutokana na namna mbalimbali mbali anavyobadilika kwenye midundo tofauti na kurapu kisasa kulingana na utandawazi unavyokwenda.

Hivyo kuna kila dalili kwa Konde Gang kuvuna mkwanja mrefu kupitia matamasha, mauzo ya nyimbo na matukio mengine chanya atakayoyafanya wakali hao akiwamo Killy na Cheed walitambulishwa vyema katika fani ya muziki na mfalme Alikiba kabla ya kujiengua Kings Music.