Gabo: Safari ya kwenda tuzo za Oscar imekaribia

Muktasari:

Namna anavyojisikia baada ya filamu yake ya ‘Siyabonga’ kuingia katika mtandao wa kuuza filamu za wasanii wa wa hapa nchini ya Swahiliflix.

Dar es Salaam.Mchezafilamu Gabo amesema anaiona safari yake ya kuelekea tuzo za Oscar inavyokwenda kukamilika.

Gabo jina lake halisi ni Ahmed Salim ameyasema hayo katika mahojiano na Mwanaspoti iliyotaka kujua namna anavyojisikia baada ya filamu yake ya ‘Siyabonga’ kuingia katika mtandao wa kuuza filamu za wasanii wa wa hapa nchini ya Swahiliflix.

Uzinduzi wa huo wa Siyabonga, ulifanyika katika ukumbi wa Mlimani City, na kuhudhuriwa na wasanii mbalimbali akiwemo Yusufu Mlela, Jacquie Wolper, Ebitoke, Hamisa Mobeto, Ray na Chuchu Hans.

Gabo aliyewahi kushinda tuzo mbalimbali ikiwemo ya msanii bora wa kiume mara nne, akuzungumzia hatua hiyo, alisema kupitia mtandao huo, anaamini kazi yake itakwenda mbali duniani.

‘Tulishazoea kazi zetu zinaishia hapa nchini, lakini kutokana na kukua kwa teknolojia na kupata jukwaa  kama hili la Swahiliflix la kuuza kazi zetu ni wazi zitakwenda mbali duniani na kuonwa na wale wanaoandaa tuzo za kimataifa ikiwemo Oscar.

‘Sasa naweza kusema ile safari yangu ya kuelekea kushinda tuzo za Oscar inakaribia kwa hatua hii niliyofikia kikubwa niwaombe mashabiki zangu waendelee kinipa sapoti yao ili kufika huko,”alisema.

Hata hivyo alisema anashukuru ‘Siyabonga’ ni filamu ambayo imepokelewa kama ambavyo yeye na timu yake walidhamiria iwe kazi kubwa.

Alisema hilo limejidhihirisha kwani wakati ikiwa haijazinduliwa rasmi iliweza kushinda kipengele cha filamu yenye maudhui ya kitaifa katika tuzo za Sinema zetu(SZIFF 2018).

Kama haitoitoshi ndio hivyo Swahiliflix imeeingiza katika mtandao wao kwa ajili ya kuiuza.