Faiza sasa aitamani ndoa

Mfanyabiashara Faiza Ally ambaye pia ni mzazi mwenzake wa mgombea wa ubunge wa Mbeya Mjini kupitia Chadema, Jospeh Mbilinyi ‘Sugu’ amesema anatamani kuwa na ndoa kwa sasa.

 

Kupitia video aliyoiweka kwenye akaunti yake ya Instagram leo Oktoba 21,  Faiza amesema kwa mara ya kwanza katika maisha yake anatamani kuwa na mume ili amsaidie ikiwemo kwenye mambo ya biashara.

 

“Kwa mara ya kwanza nimetamani kuwa na mume au rafiki wa karibu kwa sababu kuna mtu nilifanya naye baishara namdai, lakini ananisumbua kwa muda mrefu na anafanya hivyo kwa sababu anajua sina mume ambaye naweza kwenda naye kwake kudai haki yangu,” amesikika akisema Faiza kwenye video hiyo.

 

Ameongeza kuwa hayuko singo kwa sasa, lakini mpenzi wake yuko mbali akidai kuwa yuko nje ya nchi na hatarajii kurudi hivi karibuni.

 

Ila, pia amejaribu kuwatafuta kaka zake wote na kuomba wakamsaidie kudai lakini wamemueleza kuwa wapo bize.

 

Aidha, Faiza amegoma kumtaja mdeni wake, lakini akiahidi kwamba mpaka leo jioni kama hatapata haki yake ataweka kila kitu wazi.

 

“Siwezi kumtaja mtu ninayemdai kwa sababu ni mtu maarufu, amejenga brand yake, nikimtaja nitamharibia,” amesema.

 

Faiza ni mama wa watoto wawili ambaye alijizolea umaarufu zaidi miaka ya nyuma kwa kufanya vituko mbalimbali ikiwemo kuvaaa nguo iliyochanika kwenye makalio kwenye red carpet ya tuzo za KTMA 2015 pamoja na kuvaa diaper (chupi ya mkojo ya watoto) katika siku yake ya kuzaliwa.