Asha Baraka achafukwa

 MMILIKI wa bendi ya muziki wa dansi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ na mdau  wa muda mrefu wa muziki huo, Asha Baraka ‘Iron Lady’ amechefukwa na wasanii wa muziki wa Bongofleva kwa tabia zao za kutopenda kushiriki shughuli zinazowahusu wanamuziki wa dansi.

Akizungumza katika msiba wa aliyekuwa mpiga gita la solo maarufu wa Msondo Ngoma, Saidi Mabera aliyefariki wiki hii nyumbani kwake Goba, Dar es Salaam, Asha alisema ameshangazwa kutowaona wasanii wa Bongofleva kwenye msiba huo licha ya kwamba Mabera alikuwa msanii mwenye mchango mkubwa kwenye muziki wa Tanzania kwa ujumla.

“Wazee kama kina Mabera ndio walioutengeneza huu muziki mpaka ikazaliwa hii miziki mingine ya kizazi kipya. Huyu ni mtu ni muhimu, ilitakiwa tuone wasanii wa Bongofleva wamejazana hapa kuja kutoa heshima yao ya mwisho, lakini hawapo.” alisema Asha.

Aliongeza wasanii wa kisasa wamekuwa wakijitokeza zaidi kwenye party kuliko matukio muhimu yenye historia ya muziki wao.