‘Acha Lizame Challenge’ yamponza Nandy, aitwa Basata

Muktasari:

Wimbo huo aliomshirikisha Harmonize aliuachia Juni 12, 2020 una watazamaji zaidi ya milioni tatu kwenye akaunti ya YouTube ya Nandy.

Tangu kutoka kwa wimbo wa ‘Acha lizame’ ya msanii Faustina Charles maarufu Nandy, amekuwa akiendesha shindano la kucheza wimbo huo katika akaunti yake ya mtandao wa Instagram.

Wimbo huo aliomshirikisha Harmonize aliuachia mwezi mmoja uliopita umejizolea maarufu na kufanya vizuri katika vituo mbalimbali vya redio na televisheni.

Katika kuwapa burudani mashabiki zake, Nandy kupitia ukurasa wake wa Instagram alikuwa akiendesha shindano la kucheza wimbo huo aliloliita ‘Achalizame Challenge’.

Hata hivyo jana Jumatano Julai 29, 2020 alifika Basata kuitikia wito baada ya kuitwa kutokana na video hizo ambazo zingine zilionyesha kukiuka maadili.

Akizungumza mara bada ya kutoka katika kikao hicho, Nandy amesema “Napenda kuomba samahani kwa wapenzi wangu, mshabiki zangu, wazazi na Serikali. Huko nyuma tulikuwa tunafanya promosheni ya wimbo na tulikuwa tunaposti video mbayambaya hivi, picha flani hivi ambazo zilikuwa sio za maadili”

Aliongeza “Niseme tu nimetoka Basata kwa wazazi wangu , walezi wangu na wamenishauri na wamenikumbusha, sisi  kama vijana kuna wakati  tunajisahau,  naomba niseme haitajirudia tena, nimepata maarifa makubwa, nikiwa  kama kijana ambaye napambana  ili baadaye niwe mtu mkubwa zaidi ya hpa kwa jamii yangu,naomba tuendelee kusapotiana,nawapenda sana,’amesema Nandy alipofanya mahojiano na Basata.