Neymar aanza kuivuruga PSG

Muktasari:

Mshambuliaji Brazil ndiye mchezaji ghali zaidi kwa sasa

Paris, Ufaransa. Mshambuliaji wa Brazil, Neymar ameripotiwa kuibua mapya huko PSG akidai alipwe Pauni 1 milioni kwa wiki ili abaki kwenye kikosi hicho kinachoshiriki Ligi Kuu Ufaransa.

Mshambuliaji Mbrazili alitua kwa Wafaransa hao kwenye dirisha la majira ya kiangazi lililopita kwa uhamisho wa Euro 222 milioni akitokea Barcelona, ada iliyoweka rekodi ya uhamisho duniani.

Lakini, jina lake kwa sasa linatajwa sana huko Real Madrid ambako wanamtaka akawe mrithi wa Cristiano Ronaldo, ambaye kwa sasa anaelekea miaka yake ya mwisho kwenye mchezo wa soka.

Kwa mujibu gazeti la Sunday Times, Neymar ameanza kuwatikisa PSG akitaka waongeza mshahara wake kwa kuuzidisha mara tatu kama wanataka aendelee kubaki kwenye kikosi hicho cha Paris.

Neymar haonekani kwenye mechi kwa sasa kutokana na kuuguza majeraha yake ya kufanyiwa upasuaji, baada ya kuvunjika mfupa wa uvungu wa mguu na yupo kwenye hatikati ya kukosa fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika baadaye mwaka huu huko Russia.

Matakwa hayo ya Neymar yanaripotiwa kuwa mtihani mzito kwa PSG, ambapo sasa wapo kwenye njia panda juu ya kuchukua uamuzi wa ama wampe furaha Mbrazili huyo kwa kumlipa anachokitaka au waachane naye tu aende anakotaka kwenda.