Mourinho atoa dau nono kwa Asensio

Muktasari:

Klabu hizo mbili zimekuwa na utaratibu wa kuuziana wachezaji

London, England. Manchester United ipo mbioni kutenga Pauni 177 milioni ili kuinasa saini ya mshambuliaji chipukizi wa Real Madrid, Marco Asensio.

Pia klabu hiyo imesema itaweka mezani mshahara mnono ili kupata saini ya mchezaji huyo.

Kinda huyo mwenye miaka 21 limemvutia kocha Jose Mourinho na anataka kumsajili katika usajili wa dirisha dogo Januari, mwakani.

Endapo mpango huo utakamilika mchezaji huyo atavunja rekodi ya Paul Pogba aliyetua Man United kutoka kwa ‘Kibibi Kizee’ cha Turin Juventus kwa Pauni 89 milioni.

Man United inamtaka kinda huyo wa timu ya Hispania kwa kuwa ana umri mdogo na inatarajia kumpa mkataba wa miaka mitano utakaomfunga Old Trafford.

Mchezaji huyo alicheza katika mchezo wa kimataifa dhidi ya Costa Rico ambao Hispania ilishinda mabao 5-0, Jumamosi iliyopita.