Mfaransa Migne apewa mikoba Harambee Stars

Muktasari:

  • Kocha huyo anakibarua cha kuhakikisha Kenya inacheza fainali za Mataifa ya Afrika mwakani

Nairobi, Kenya. Kocha Sebastian Migne amerithi mikoba ya Paul Put yakuwa mkufunzi mkuu wa timu ya taifa ya Kenya, Harambee Stars leo, Alhamisi Mei 03, 2018.

Kocha Migne ametangazwa leo asubuhi na Shirikisho la Soka Kenya (FKF) kuchukua mikoba iliyoachwa na Mbelgiji, Paul Put, aliyebwaga manyanga Februari 19, mwaka huu.

Nafasi hiyo ilikuwa wazi kwa muda sasa tangu kuondoka kwa Put huku msaidizi wake, Stanley Okumbi, aliyekaimu nafasi hiyo akipangiwa majukumu ya kukinoa kikosi cha U-20 kufuatia kuandikisha msururu wa matokeo yasiyoridhisha.

Moja ya sababu zilizopelekea uamuzi wa kung'atuka uliochukuliwa na Put, ikiwa ni miezi mitatu tangu akabidhiwe mikoba ya kukinoa kikosi hicho, inadaiwa kuwa ni kitendo cha FKF kushindwa kumpa watu wa kumsaidia katika majukumu yake mapema.

Mfaransa Migne amembwaga Mdachi Ruud Krol aliyekuwa akipigiwa upatu kuchukua majukumu hayo. 

Migne  aliyekuwa katika kikosi cha Togo, kama kocha msaidizi, katika mashindano ya Mataifa ya Afrika, yaliyofanyika mwaka jana.

Machi 2017, aliteuliwa kuwa Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Congo, lakini aling'atuka Machi 2018, baada ya kutorodhishwa na falsafa za shirikisho la soka nchini humo.

 Mafanikio makubwa aliyowahi kupata kama kocha ni kukiongoza kikosi cha U-20 cha Congo kushiriki mashindano ya ubingwa wa Afrika kwa vijana.

Baada ya kuteuliwa jukumu la kwanza kwa kocha mpya wa Harambee Stars, litakuwa ni kuongoza kikosi hicho katika mechi za kufuzu fainali za Mataifa ya Afrika 2019

Kenya, iliyoo katika kundi F, itakuwa mwenyeji wa Ghana kwenye mchezo wa makundi, Novemba 7, mwaka huu.