Mabosi Prisons washtukia mchezo

MABOSI wa Maafande wa Tanzania Prisons wana mkwara kinoma. Kwanza wamesema mwaka huu lazima kieleweke, kisha wakachimba mkwara mzito.

Ishu iko hivi. Wakati Ligi Kuu ikiwa imemalizika, huku timu zikiwa zimeanza kufanya usajili kwa ajili ya msimu ujao, mabosi wa timu hiyo ya jijini hapa wamesema piga ua wataondoka wachezaji wote ila sio wa safu ya ulinzi.

Wamesema kamwe hawawezi kuwabania wale watakaopata dili timu nyingine, lakini wakikutana tu na maombi ya wachezaji wake wa safu ya ulinzi, watayatupa kapuni fasta.

Safu ya ulinzi ya Maafande hao inaongozwa na Laurian Mpalile, Jumanne Elphadhili, James Mwasote, Salum Kimenya, Nurdin Chona na kipa Aron Kalambo.

Katibu Mkuu wa Prisons, Havintish Abdalah ameliambia Mwanaspoti baadhi ya wachezaji tayari wamenaswa na klabu zingine kwa ajili ya msimu ujao, lakini nafasi zao zinazibika fasta tu na wachezaji makinda kutoka kikosi cha pili.

“Piga ua, safu ya ulinzi hii haitatoka hapa, itabaki kama ilivyo kwani imekuwa ikifanya shughuli kubwa uwanjani. Lakini maeneo mengine ambayo wachezaji wake wanaweza kuondoka tunaweza kuziziba bila kufanya usajili,” alisema.