Casto Dickson awafungia kioo wanaomponda Tunda, atangaza ndoa

Muktasari:

Amesema amekutana na wanawake wengi lakini kwa Tunda amekuta vitu tofauti.

Dar es Salaam. Mtangazaji wa kipindi cha Siz Kitaa cha Clouds TV, Casto Dickson, anatarajia kufunga ndoa na video queen, Anna Kimario 'Tunda' kabla ya mwaka kwisha.

 

Akizungumza na MCL Digital, Dickson amesema atafanya hivyo kwa kuwa ndio mwanamke anayeona anafaa kuwa mke.

 

"Unajua nimekuwa na mahusiano na wanawake wengi, lakini kwa Tunda nimekuta vitu tofauti sana, kwangu namuona anafaa kuwa mke wa mtu tofauti na watu wa nje mnavyomuona na nitamuoa kabla huu mwaka haujaisha," amesema mtangazaji huyo.

 

Amesema watu wamekuwa wakihoji iweje niwe na mwanamke ambaye ameshawahi kuwa na mahusiano na wanaume wengine, nawaambia wanamuona hivyo kwa kuwa ni maarufu lakini ukweli ni kwamba kuna watu wa kawaida wameshawahi kuwa na idadi ya wanaume wengi kuliko hata Tunda.

 

"Halafu kila unapoanza mahusiano na mtu ukataka kujua historia ya wanaume aliowahi kuwa nao, yatakushinda. Unachopaswa kuangalia kuanzia hapo mlipokutana na namna ya kwenda mbele kwani hata mimi nilishakuwa nao wengi kabla ya kukutana na Tunda," ameeleza Dickson.