Rose Ndauka: Jamani zaeni

ROSE Ndauka ambaye ni mama anayetamba kwenye filamu za Bongo, amewaonya wasanii wa kike kuachana na biashara ya utoaji mimba kwani ni kinyume cha maadili na kujidhalilisha.

Alisema kuwa baadhi ya wasanii wa filamu nyota hawataki kuzaa hata wale waliozaa kabla ya kuwa nyota hawapendi kujulikana kama wamezaa, kitu ambacho hakina maana katika maisha ya msanii bali ni kujichelewesha tu.

“Mimi sijui ni kwa nini baadhi ya mastaa hawataki kuzaa, ni suala la kujipanga tu, kama una kipaji kipo tu hakiwezi kupotea sababu eti ya kuzaa,” alisema Rose na kuongeza kuwa kadri umri unavyokwenda na fursa ya kuzaa inapotea na wengi hawajui umuhimu wa kuzaa mapema.

Ingawa anasema kuna woga wa majukumu ya kulea kwa baadhi ya vijana wa kisasa na si wasanii peke yao. Rose hivi karibuni alijifungua mtoto wa kike na kumpa jina la Naveen.