Zahera afunguka mazito kwa straika mpya Yanga!

Muktasari:

Mwanaspoti lilizungumza na Zahera kutaka kujua sababu kubwa ya kumuongeza Falcao katika dakika za mwisho kabla dirisha la usajili halijafungwa.


KOCHA Mwinyi Zahera wa Yanga, ameweka wazi sababu ya kumsajili mshambuliaji David Molinga Ndama ‘Falcao’ katika kikosi chake.

Usajili wa mchezaji huyo ulifanyika nyakati za mwisho -tena kwa kumkata kipa Klaus Kindoki na ndipo Falcao akatua katika kikosi hiko.

Mwanaspoti lilizungumza na Zahera kutaka kujua sababu kubwa ya kumuongeza Falcao katika dakika za mwisho kabla dirisha la usajili halijafungwa.

Zahera alisema katika usajili wake alisajili mshambuliaji mmoja tu ((Sadney) ambaye kazi yake ni kutupia nyavuni hivyo ilimlazimu kuongeza mtu mwingine.

“Sina washambuliaji wengi, nina Sadney na huyu Falcao. Balinya ni namba kumi lakini anaweza kucheza kama kiungo ni sawa na Kalengo ambaye ni winga licha ya kuweza kucheza kama mshambuliaji,” alisema.

Akizungumzia uwezo wa Falcao alisema katika msimu uliopita alikosa mtu ambaye alikuwa na spidi na uwezo wa kupambana, ndio maana ameamua kumsajili Falcao.

“Mara kwa mara nilikuwa namwambia (Herietier) Makambo kuwa licha kufunga lakini hana spidi, hakuwa mtu wa kupiga chenga na kwenda kufunga ndio maana nimemleta Falcao, nilikuwa namwambia hata yeye.”

Alisema katika upande wa spidi nyota huyo mpya ana kasi na ndio jambo ambalo alikuwa analiangalia katika usajili wake mpya.

“Falcao anajua kufunga, kupambana na spidi. Kwa hiyo naamini atafanya vizuri, kwa upande wa mawinga pia kuna wachezaji wapya ambao wana kasi na wanajua kupiga krosi sahihi, hivyo, hakuna wasiwasi,” alisema.

Aliongeza kuwa mpira wake ni wa mbio, mshambuliaji wake Falcao ana uwezo huo huku Sadney akiwa na uwezo mkubwa wa kumtoka beki pindi wanapokuwa pamoja.