Yanga yawapigia hesabu Kagera Sugar Dar
Muktasari:
Kocha wa Yanga, Zlatko Krmpotic anaendelea kukisuka kikosi chake kuhakikisha kinakuwa mwiba kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL), ndio maana siku tatu za mapumziko kuisubiri Kagera Sugar, anajipima ubavu na Mlandege.
YANGA haitaki kupoa baada ya kutoka kuvuna pointi tatu dhidi ya Mbeya City, kesho Jumatano inajipima ubavu na Mlandege ya Zanzibar, mchezo utakaopigwa saa 1:00 jioni.
Imeelezwa kwamba kocha wa timu hiyo, Zlatko Krmpotic anahitaji wachezaji wapate mechi nyingi zitakazowasaidia kuzoeana, ndio maana ameona siku siku tatu ambazo wanapumzika kusubiria mechi na Kagera Sugar, ijipime na Mlandege, Uwanja wa Chamazi Complex.
"Mechi hiyo inachezwa kwa mambo mawili, wachezaji kupata muda wa kuzoeana, pia uwanja wa Kagera Sugar unatumia nyasi bandia, ndio maana akataka wazoee kwa kucheza Uwanja wa Azam Complex," amesema mmoja wa kiongozi wa Yanga ambaye hakutaka kutajwa jina lake.
Ameongeza kuwa "Kocha amesema anahitaji timu iwe na mechi nyingi, ili apate kombinesheni ya wachezaji itakayokuwa tishio kwa timu pinzani, kwani anaamini kikosi chake ni kizuri,"amesema.
Si mara ya kwanza Yanga SC kucheza na Mlandege, ikiwa chini ya Mwinyi Zahera, iliifunga timu hiyo mabao 4-1 mechi hiyo ilichezwa usiku Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Kikosi cha Yanga kilichocheza mechi hiyo chini ya Zahera kilikuwa na Farouk Shikhalo/Metacha Mnata, Paul Godfery/Cleophas Sospeter, Muharami Issa ‘Marcelo’/Jaffar Mohamed, Ally Mtoni ‘Sonso’/Ally Ally.
Wengine ni Lamine Moro/Moustafa Suleiman, Papy Tshishimbi/Abdulaziz Makame, Mapinduzi Balama/Mrisho Ngassa, Mohammed Issa ‘Banka’/Feisal Salum, Sadney Urikhob/Maybin Kalengo, Juma Balinya/Issa Bigirimana na Patrick Sibomana/Deus Kaseke.