Winga Alliance akomaa na sarakasi

Muktasari:

  • Richard ndio mchezaji anayeongoza kwa ufungaji mabao ndani ya kikosi cha Alliance ambapo amepachika bao Sita mpaka sasa ligi kuu akifatiwa na Jerryson Tegete mwenye mawili.

WINGA wa Alliance FC,David Richard amesema itachukua muda mrefu kuacha kushangilia kwa staili ya kuruka sarakasi ambaye amekuwa akishauriwa kuiacha na watu mbalimbali kwa kuwa inaweza kumumiza.

Akizungumza na Mwanaspoti Online, Richard(20) alisema ni jambo gumu kwake kuacha kushangilia kwa staili hiyo ambapo amesema alishazoea tangu anaanza kucheza soka hivyo kuacha itachukua muda.

Alisema watu wengi wamekuwa wakimshauri kuacha kuruka sarakasi hizo ambapo amesema yeye anaporuka huwa makini sana kwani anajua madhara yake pindi atakapokosea wakati anaruka.

“Unajua haya ni mazoea yaani ile kuruka vile ndio furaha yangu hivyo kuacha kuruka sarakasi inaniwia vigumu sana ninaweza kujizuia lakini inanishinda,” alisema Richard.

Hadi sasa Alliance wako nafasi ya 18 katika msimamo wa ligi kuu wakiwa na pointi 29 huku wakiwa wamebakiza michezo tisa kumaliza mechi zake msimu huu.