Vichwa vitatu kukiwasha Arsenal

LONDON, ENGLAND. LICHA ya bajeti yake kuwa ndogo Arsenal imeingia sokoni kupambana kuwania saini ya nyota watatu, ikiwemo Memphis Depay, Raul Jimenez na Moussa Dembele katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi.

Jimenez, ambaye amefunga mabao 17 katika Ligi Kuu England msimu huu akiwa na kikosi cha Wolves, pia anawaniwa na Liverpool na Real Madrid. Arsenal inataka kumsainisha fundi huyo ili kumfanya kuwa mbadala wa Alexandre Lacazette na Pierre-Emerick Aubameyang.

Lakini, ripoti zinadai kuwa anaweza kuendelea kusalia klabuni hapo kwa kuwa ni mmoja kati ya wachezaji muhimu na Wolves itakuwa ngumu kumuachia kirahisi.

Mbali na klabu hizo Manchester United na Barcelona pia zipo kwenye harakati za kuhakikisha inaipata saini ya straika huyo kutoka Mexico.

Arsenal pia ipo kwenye harakati za kumsainisha Depay, ambaye amemaliza msimu wa Ligi Kuu Ufaransa akiwa na Lyon kwa kufunga mabao 14 na kutoa asisti mbili katika mechi 18.

Pia, inataka kumsajili Dembele anayecheza hapo hapo Lyon, ambaye amefunga mabao 25 na kutoa asisti 10 katika michuano yote. Akionekana kuwa mchezaji pekee mwenye rekodi bomba katika orodha hiyo ambayo Arsenal inataka kuhakikisha inawasajili ili kuboresha kikosi kwa msimu ujao.