Unai Emery awa mkali kisa Jose Mourinho

Muktasari:
Mourinho alionekana uwanjani Emirates wakati Arsenal ilipomenyana na Vitoria mwezi uliopita na kushinda kwa mbinde 3-2.
LONDON ,ENGLAND . KOCHA Unai Emery amekuwa mbogo kwa mwandishi aliyemuuliza kuhusu uwezekano wa kibarua chake kuchukuliwa na Jose Mourinho huko Arsenal.
Kocha Mourinho amekuwa hana kazi tangu alipoondolewa Manchester United, Desemba 2018 na siku za karibuni amekuwa akihusishwa na kibarua cha kwenda Arsenal na Bayern Munich.
Mourinho alionekana uwanjani Emirates wakati Arsenal ilipomenyana na Vitoria mwezi uliopita na kushinda kwa mbinde 3-2.
Juzi Jumatano, kikosi hicho kilipoteza tena uongozi wake wa bao 1-0 uwanjani na kutoka sare na Vitoria katika mchezo wa marudiano wa Europa League na kukiweka kwenye hatari kubwa kibarua cha Mhispaniola huyo.
Emery aliulizwa kama haogopi kufukuzwa kazi, ambapo kwa hasira alijibu: “Mimi ndio kocha hapa.”
Jambo hilo limekuja baada ya Arsenal kuonekana kuwa na tatizo katika siku za karibuni, ambapo imekuwa ikifunga mabao na kuzifanya timu pinzani kurudisha, ilikuwa hivyo kwenye mechi kibao zilizopita. Katika mchezo huo wa Vitoria, Arsenal ilipiga pasi 579, lakini zote hizo zilikuwa kwenye eneo la katikati na kwao, haikufanya hivyo ndani ya boksi la Vitoria.