Ukatibu RT sasa kwa ajira tu

Muktasari:

Ikangaa alisema kama RT ikiajiri mtendaji, miiko ya utendaji itakuwepo kwa kuwa atakuwa kwenye ajira kama ajira nyingine na ataheshimu kazi yake.

SIKU chache baada ya aliyekuwa katibu mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday kujiuzulu ghafla, rais wa RT, Anthony Mtaka amefichua kuwa kuanza sasa nafasi ya ukatibu mkuu itakuwa ya kuajiriwa na si kugombewa.

Mtaka amebainisha hilo, akisema wanataka nafasi ya mtendaji iwe ya kuajiriwa na si kugombea kupitiwa uchaguzi mkuu, nia ikiwa ni kutaka ufanisi zaidi kwa maendeleo ya mchezo huo.

“Mchakato wa kupata katibu mkuu utaanza karibuni, tutatangaza nafasi ya kazi na kuanzia hapo mtendaji mkuu wa RT atakuwa ni mwajiriwa,” alisema.

Awali nafasi hiyo ilikuwa ikipigiwa kura kwenye uchaguzi mkuu na Gidabuday aliichukua Novemba 2016.

Juzi jumatatu wanariadha nguli wa zamani, Filbert Bayi na Juma Ikangaa katika mahojiano na gazeti hili walieleza umuhimu wa RT kuwa na mtendaji wa kuajiriwa.

Ikangaa alisema kama RT ikiajiri mtendaji, miiko ya utendaji itakuwepo kwa kuwa atakuwa kwenye ajira kama ajira nyingine na ataheshimu kazi yake.

Bayi alisema kuajiri katibu mkuu ndiyo njia nzuri ya uwajibikaji.

Gidabuday alijiuzulu ikiwa saa chache baada ya kikao cha pamoja kati ya viongozi wa RT na Waziri wa Michezo, Dk Harrison Mwakyembe kwa madai ya masilahi ya mchezo huo.

Wakati huohuo, Mtaka amewapongeza wanariadha walioshiriki mashindano ya majeshi ya dunia hivi karibuni nchini China.

Mtaka alikula chakula na wanariadha hao katika hafla fupi iliyofanyika Jumatatu usiku kwenye hoteli ya Regency, Dar es Salaam.