Solskjaer amvuta kipa Mcameroon kuziba pengo la De Gea

Muktasari:

 Matumaini ya De Gea kubaki Man United ni hafifu kwa kuwa amebakiza miezi 12 kabla ya mkataba wake kumalizika. 

London, England. Manchester United inamsaka kipa namba moja wa Ajax Amsterdam ya Uholanzi, Andre Onana kurithi mikoba ya David De Gea.

Man United inaamini kipa huyo ana kiwango bora cha kuvaa viatu vya David de Gea anayehusishwa na mpango wa kujiunga na Real Madrid.

Kipa huyo namba moja wa Hispania ameweka ngumu kutia saini mkataba mpya akitaka nyongeza ya mshahara.

Matumaini ya De Gea kubaki Man United ni hafifu kwa kuwa amebakiza miezi 12 kabla ya mkataba wake kumalizika.

Hata hivyo, Man United italazimika kuvunja benki kupata saini yake kwa kuwa anauzwa Pauni40 milioni.

Mtendaji Mkuu wa Man United, Ed Woodward amedai ataingia sokoni kusaka wachezaji hodari ambao watarejesha heshima ya klabu hiyo iliyopoteza katika miaka ya hivi karibuni.

Mbali na Onana, kipa wa Atletico Madrid, Jan Oblak anahusishwa na mpango wa kutua Old Trafford majira ya kiangazi.

Lakini, Onana mwenye miaka 23 na kipa namba moja wa Cameroon ameonekana ni chaguo la kwanza kwa kocha Ole Gunner Solskjaer.