Simba kutesti mitambo Kigoma

Muktasari:

Simba itacheza na Mashujaa Oktoba 9 huku mchezo wao dhidi ya Aigle Fc wakicheza Oktoba 11 zote mkoani Kigoma.

VINARA wa Ligi Kuu, Simba imepanga kupima makali yao kwa kucheza michezo miwili ya kirafiki dhidi ya Mashujaa Fc (Kigoma) na Aigle (Burundi)  ili kujiweka fiti kabla ya kuvaana na Azam FC kwenye mfululizo wa ligi.
Simba na Azam zitacheza mchezo wao wa Ligi Kuu Oktoba 23, wakati huo huo Azam watacheza mchezo wao wa mwisho leo dhidi ya Namungo Fc na baada ya hapo watasimama kupisha timu ya Taifa.
Kwa upande wa Simba tangu wametoka kucheza na Biashara Utd, hawajacheza mchezo wowote baada ya ule dhidi ya KMC kuhailishwa hivyo wameamua kucheza mechi za kirafiki mbili.
Kocha Patrick Aussems alisema kikosi chake kitacheza michezo miwili ya kirafiki kwaajili ya kuwaweka sawa wachezaji wake ambao watasalia katika kikosi hicho.
"Wachezaji ambao wamebaki na timu hawajaenda katika timu za Taifa watacheza mechi za kirafiki, ili wao pia wawe sawa na wale ambao wapo katika timu zao za Taifa," alisema.
Simba itacheza na Mashujaa Oktoba 9 huku mchezo wao dhidi ya Aigle Fc wakicheza Oktoba 11 zote mkoani Kigoma.