Simba, Yanga zatikisha ndani, nje Ligi Kuu Bara

Muktasari:

Simba na Yanga ndio timu ambazo mara kwa mara zimekuwa zikishika na kutikisa dirisha la usajili kwani ndizo zimekuwa na misuli imara ya kiuchumi.

 

Dar es Salaam. Ligi Kuu Tanzania Bara inaelekea ukingoni  ingawa zipo timu zimecheza mechi chache zaidi ya hizo kutokana na kuwa na viporo ambavyo vilitokana na ratiba zao kubadilishwa na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB).

Simba na Yanga ndio timu ambazo mara kwa mara zimekuwa zikishika na kutikisa dirisha la usajili kwani ndizo zimekuwa na misuli imara ya kiuchumi.

Pindi itakapomalizika Ligi Kuu msimu huu ni mwanzo wa maandalizi kwa ajili ya msimu ujao kwani kunatoa fursa kwa timu kuanza kufanya usajili na kuingia kwenye kambi za mazoezi ili ziwe na vikosi imara vyenye ushindani msimu ujao.

Kwa wachezaji, ligi inapomalizika inaweza ikawa neema kwao kwa kuwa wanaweza kuvuna kiasi kikubwa cha fedha za usajili watakapojiunga na klabu nyingine au kuongeza mikataba kwenye timu wanazocheza.

Lakini kuna wale ambao huenda kikawa kipindi kigumu kwao kukosa timu za kuwasajili ama kutemwa na klabu zao kutokana na kiwango duni ambacho wamekionyesha msimu huu, lakini hayo yote yatategemeana na ripoti zitakazowasilishwa na makocha wa timu zao.