Sadio Mane ampamba Klopp kwa ubora

Muktasari:

Staa Mane amekuwa sehemu muhimu ya mafanikio hayo na kutajwa kuwa mmoja wa wanasoka bora kabisa duniani akijumuishwa kwenye orodha ya wanaofukuzia tuzo ya Ballon D’Or mwaka huu.

LIVERPOOL, ENGLAND . STAA, Sadio Mane amesema Jurgen Klopp ndiye kocha bora zaidi duniani kwa sasa akisifu anavyowasimamia wachezaji wake na anavyowapa mbinu na ujanja wa kuwatesa wapinzani uwanjani.

Mane alikuwa mmoja wa usajili wa kwanza kabisa kufanywa na kocha Klopp baada ya kutua Liverpool, ambapo fowadi huyo alikuwa huko Southampton na aliwasili Anfield kwa ada ya Pauni 34 milioni mwaka 2016.

Na tangu wakati huo, klabu, kocha na mchezaji wote wameonekana kuwa bora katika mambo mengi tofauti ya kimpira. Klopp aliongoza Liverpool kubeba ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu uliopita huku msimu huu kikosi hicho kikiongoza kwa pointi nane kwenye Ligi Kuu England.

Staa Mane amekuwa sehemu muhimu ya mafanikio hayo na kutajwa kuwa mmoja wa wanasoka bora kabisa duniani akijumuishwa kwenye orodha ya wanaofukuzia tuzo ya Ballon D’Or mwaka huu.

“Sijui nieleze vipi kuhusu mafanikio yake aliyopata hapa Liverpool,” alisema Mane akimzungumzia Klopp. Kila mtu anaweza kuona kile alichokifanya kwenye timu hiyo, jinsi alivyoonyesha ubora wake. Kuna makocha wengi sana Ulaya, lakini ninachoweza kusema kuhusu kocha wetu, maneno sahihi na kile ambacho anakifanya kwenye timu na anavyoingoza, ninaweza kusema ni bora zaidi duniani.”

Mane, ambaye alishinda Kiatu cha Dhahabu kwenye Ligi Kuu England msimu uliopita sambamba na mastaa wengine, Mohamed Salah, anayecheza naye timu moja na Pierre-Emerick Aubameyang wa Arsenal msimu uliopita, kwa sasa ndiye kinara wa mabao wa Liverpool kwa msimu huu akiwa amefunga mabao 11. Na fowadi yote ya Liverpool inayoundwa na wakali Mane, Salah na Roberto Firmino imefunga mabao 182 tangu 2017/18 hadi sasa.