Ray C hataki mpenzi eti yupo singo

BAADA ya kimya cha muda mrefu na kuhusishwa na matumizi ya madaya wa kulevya, hatimaye nyota wa Bongo Fleva, Rehema Chalamila ‘Ray C’ ameibukia Kwa Malkia Queen Elizabeth kule Uingereza.

Ray C maarufu kama Kiuno Bila Mfupa kutokana na uwezo wake wa kuzungusha nyonga hajaibuka hivihivi, bali amejipanga na kurudi upya kwenye fani.

Akizungumza kutokea England, Ray C amedai kwa sasa anafikiria zaidi maisha yake ya muziki na wala hawazi suala la mapenzi.

“Sina mpenzi,” alisema Ray C na kuongeza: “Kwa sasa nafikiria kuhusu muziki wangu sitaki kujichanganya na mambo mengine.­­­ Mashabiki wangu wamenipambania kwa muda mrefu siyo kwa ajili ya mpenzi wangu, wao wanataka kazi, muziki mzuri.”

Aidha mwimbaji huyo ambaye kwa sasa anafanya vizuri na  wimbo wake mpya ‘Unanimaliza’ alijibu tuhuma za kutafuta kiki kupitia Hamisa Mobetto kutokana na kupinga kila anachoposti mwanamitindo huyo kwenye mitandao ya kijamii

“Kwanza watu wafahamu sina ugomvi na Hamisa, nimejikuta tu nafananishwa naye kuwa amenizidi kwa kila kitu,wakati katika kurasa zangu za mitandao huwa najiandikia tu maneno yangu.

“Maneno mengine yakimgusa ndio watu wanahisi amelengwa mtu, lakini huwa simlengi Hamisa kama watu wanavyodhani, lakini pia watu waelewe kila mtu ana uhuru wa kufanya anachotaka., na kuwa muwazi pale unapoona mambo fulani hayajakaa sawa,” alifafanua Ray C.

 Ray C ambaye aliwahi kufanya vizuri miaka ya nyuma na wimbo wake wa ‘Mapenzi Matamu’, alikuwa kimya kwa muda mrefu akijaribu kuachana na matumizi ya madawa ya kulevya ambayo yalimuathiri kwa kiasi kikubwa.