Rashford : Ole anafaa jamani mwacheni

Muktasari:

Akizungumzia mkataba wake wa sasa ambao utafika tamati 2023, Rashford alisema hakusita juu ya mpango wa kusaini mkataba mpya kwenye timu hiyo ili kuendelea kubaki hapo kwa miaka mingi kitu ambacho anaamini kitakuwa hivyo pia kwa Ole.

MANCHESTER, ENGLAND . STAA wa Manchester United, Marcus Rashford ana uhakika kwamba Ole Gunnar Solskjaer bado ni mtu mwafaka wa kuiongoza timu hiyo licha ya kuwapo kwa kocha Mauricio Pochettino.
Kocha Pochettino baada ya kufutwa kazi Tottenham Hotspur sasa anapewa nafasi kubwa ya kwenda kuchukua mikoba ya kuinoa Man United baada ya Solskjaer kuonekana kwamba amepewa kazi nzito kuliko uwezo wake.
Lakini, fowadi wa timu hiyo na timu ya taifa ya England. Rashford - ambaye kwa sasa anaonekana kucheza soka la ubora mkubwa anaamini Solskjaer bado ni mtu sahihi wa kuendelea kuitumikia timu hiyo ya Old Trafford.
Alisema: “Ole ni mtu safi na klabu anaipenda toka moyoni. Hakuna mtu mwingine bora kwa kibarua hiki.”
Akizungumzia mkataba wake wa sasa ambao utafika tamati 2023, Rashford alisema hakusita juu ya mpango wa kusaini mkataba mpya kwenye timu hiyo ili kuendelea kubaki hapo kwa miaka mingi kitu ambacho anaamini kitakuwa hivyo pia kwa Ole.
Baada ya mechi 12 zilizochezwa kwenye Ligi Kuu England, Man United wanashika nafasi ya saba katika msimamo, pointi tisa nyuma ya timu inayoshika nafasi ya nne.
Lakini, bado wana nafasi ya kubeba mataji msimu huu baada ya kuendelea kufanya vizuri kwenye Europa League, Kombe la FA na Kombe la Ligi.
“Kama tutamaliza msimu huu ndani ya Top Four na kisha hatujabeba taji sitakuwa na furaha kabisa," alisema Rashford.
Man United watakipiga na Sheffield United kwenye Ligi Kuu England kesho Jumapili.