Prisons yapewa basi jipya

Muktasari:

  • Prisons inashika nafasi ya tisa (9) katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa na pointi 40 ambazo imekusanya katika michezo 28, ikipata ushindi mara 9, sare mara 13 na kupoteza michezo saba

Uongozi wa Jeshi la Magereza Tanzania,leo umeikabidhi basi dogo la kisasa lenye thamani ya aidi ya Shilingi 75 milioni timu ya Tanzania Prisons inayomilikiwa na Jeshi hilo, katika hafla fupi iliyofanyika mkoani Dodoma.

Akizungumza katika makabidhiano ya gari hilo, Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Suleiman Mzee amesema kuwa kwa muda mrefu Klabu hiyo haikuwa na usafiri hivyo iliwalazimu Uongozi wa Klabu kukodi magari jambo lililochangia kuongeza gharama za uendeshaji wa Klabu.

"Nimefanya maamuzi ya kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa  changamoto ya usafiri kwa timu yetu na katika kupunguza gharama za kukodi magari hivyo nimewapatia basi dogo jipya ili waweze kulitumia kwenda sehemu mbalimbali nchini kwa mujibu wa ratiba za Ligi Kuu", amesema Kamishna Jenerali Mzee.

Mkuu wa idara ya michezo katika Jeshi la Magereza Tanzania, SSP Matlida Mlawa alisema kuwa usafiri huo utasaidia kwa kiasi kikubwa timu ya Prisons katika usafiri.

"Tunamshukuru sana Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza Afande Suleiman Mzee. Kwa kuiwezesha klabu ya Tanzania Prisons kupata usafiri ambao utaiwezesha timu kusafiri kwenda sehemu mbalimbali kucheza mechi kwa mujibu wa ratiba ya ligi.

Kwa niaba ya klabu tunapenda kumshukuru sana na tuna imani naye kwamba ataleta mabadiliko makubwa katika klabu ya Prisons," alisema SSP Mlawa.

Katika msimu huu wa Ligi, Prisons imebakiza jumla ya mechi nane ambapo kati ya hizo tano (5) itacheza ugenini dhidi ya Mwadui, KMC, Namungo, Ndanda na Singida United na nyumbani imebakiza mechi tatu (3) dhidi ya Polisi Tanzania, Azam na Coastal Union

ilianzishwa mwaka 1996 na imekuwa na historia kubwa katika tasnia ya mchezo wa mpira wa miguu nchini ambapo Mwaka 1998 iliweza kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara