Pesa yako tu kumpata Kiduku

STRAIKA Kelvin Sabato 'Kiduku' amesema amemaliza mkataba wa miezi sita aliojiunga na Kagera Sugar akitokea Gwambina FC ambapo amedai hana mpango wa kuongoza mkataba mwingine kikosini hapo.

Sasa mchezaji huyo amefungua milango kwa klabu yoyote itakayohitaji huduma yake kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

Akizungumza na Mwanaspoti Online leo Jumatano Agosti 12, 2020 Kiduku amesema anachokiangalia ni masilahi tu ambayo atapewa na timu husika huku akibainisha hana mpango wa kuendelea na Kagera Sugar.

"Msimu uliopita nilianza na Gwambina kabla ya kuondoka hapo na kwenda Kagera Sugar ambayo wakati huu nimemaliza mkataba nayo, natamani kutafuta changamoto timu nyingine hata kama ikiwa Ligi Daraja La Pili ila kikubwa maslahi yawe mazuri tu,"

"Ujua si kama nacheza katika timu kwa muda mfupi ndio maana mpaka sasa nimezitumikia timu nyingi bali natafuta maslahi ambayo natamani kuyapata ili nikimaliza maisha yangu ya soka nisije kuchekwa kuwa nimecheza mpira kwa muda mrefu halafu sina kitu,"

"Sijafanya mazungumzo na timu yoyote ile mpaka sasa ila sitarudi Kagera Sugar kwani nahitaji changamoto mpya, naamini muda si mrefu nitapata timu nyingine kutokana na mipango ambayo ninayo," amesema Kiduku aliyemaliza msimu akiwa na mabao nane