Penalti Tunisia zaivuruga Ghana

Muktasari:

Awali, Tunisia ilitangulia kupata bao dakika ya 73 lililofungwa na Taha Khenissi kabla ya mchezaji aliyetokea benchi Rami Bedoui kujifunga kwa mpira wa kichwa wakati akiokoa hatari langoni mwake.

Cairo, Misri. Kocha wa Ghana, Kwesi Appiah amesema licha ya kufanya mazoezi ya penalti, lakini wameng’olewa kwa matuta dhidi ya Tunisia juzi usiku.

Appiah alidokeza ameshangazwa Ghana kufungwa kwa penalti, lakini hana namna. Timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1 kabla ya Tunisia kupata ushindi wa mabao 5-4 kwa penalti.

Kipa wa Tunisia, Farouk Ben Mustapha alikuwa shujaa baada ya kuokoa penalti ya mwisho iliyopigwa Caleb Ekuban.

Lakini, Ferjani Sassi aliipeleka Tunisia robo fainali baada ya kiki yake ya mwisho kujaa wavuni langoni mwa Ghana.

Awali, Tunisia ilitangulia kupata bao dakika ya 73 lililofungwa na Taha Khenissi kabla ya mchezaji aliyetokea benchi Rami Bedoui kujifunga kwa mpira wa kichwa wakati akiokoa hatari langoni mwake.

“Ghana imekuwa ikitolewa sana kwa penalti katika michuano mingi, lakini tumekuwa tukifanyia mazoezi eneo hili. Tulipokuwa Dubai tulifanya sana mazoezi ya kupiga penalti,”alisema Appiah.

Mara ya mwisho Ghana kutwaa ubingwa wa Afrika kwa penalti ilikuwa mwaka 1982 iliposhinda mabao 7-6 dhidi ya Libya baada ya kutoka sare ya bao 1-1.