Nyota wa Bafana Bafana auawa kwa kupigwa risasi

Muktasari:

Mchezaji huyo ameuwawa akiwa katika gari nyumbani kwake na wauaji hawakuchukua kitu chochote

Jo’Burg, Afrika Kusini. Nyota wa zamani wa timu ya taifa ya Afrika Kusini ‘Bafana Bafana’, Marc Batchelor ameuwawa kwa kupigwa risasi nyumbani kwake jijini Johannesburg.

Batchelor mchezaji wa zamani wa Kaizer Chiefs, Orlando Pirates na Mamelodi Sundowns za Afrika Kusini alishambuliwa kwa risasi wakati anaingia nyumbani kwake na watu wawili waliokuwa kwenye bodaboda.

Msemaji wa polisi Lungelo Dlamini aliviambia vyombo vya habari kuwa Batchelor alishambuliwa na watu wawili waliokuwa akiendesha bodaboda.

"Alishambuliwa wakati alipokuwa akiingia nyumbani kwake. Washambuliaji hao walirusha risasi nyingi katika kioo cha mbele alipokuwa amekaa."

Dlamini alisema: "Alifariki akiwa ndani ya gari yake, lakini wauaji hao hawakuchukua kitu chochote.

"Kwa sasa bado tunaendelea na uchunguzi kujua nini kilichosababisha kutokea kwa tukio hili na kuwatafuta waalifu."