Mwashuiya anasubiri simu tu

Muktasari:

  • Kwa upande wa Mwashuiya anasema kuna timu nyingi zinamuhitaji lakini anasubiri simu ya Lwandamina ili kujua hatma yake.

WINGA wa Singida United, Geofrey Mwashiuya huenda akaachana na timu hiyo baada ya kushindwa kumpa stahihiki zake ambazo ni mishahara ya miezi saba na kiasi cha pesa ya usajili wake ambacho kimebaki.
Singida ilimsajili Mwashuiya mwanzoni mwa msimu huu akitokea Yanga kwa mkataba wa miaka miwili ambao ameutumikia mwaka mmoja na sasa umebaki msimu mmoja.
Mwashuiya ambaye anadaiwa kupata dili mpya Zambia katika klabu ya Zesco inayofundishwa na kocha wa zamani wa Yanga, George Lwandamina.
Mmoja wa mtu wa karibu na Mwashuiya alisema mchezaji huyo amekuwa na mawasiliano ya karibu na Lwandamina ambaye amemwambia asisaini kwanza mkataba mpaka atakapompigia simu na kumruhusu.
“Mwashuiya amewasiliana na Lwandamina na kuambiwa atulie kwanza anamtafutia nafasi Zesco na kama itawezekana atamwambia aende huko lakini ikishindikana vile vile atampigia simu na kumwambia asaini timu nyingine,” alisema
Kwa upande wa Mwashuiya anasema kuna timu nyingi zinamuhitaji lakini anasubiri simu ya Lwandamina ili kujua hatma yake.
“Kama Lwandamina akinipigia na kuniambia nikasaini Zesco naondoka, naenda kucheza mpira huko lakini akiniambia tofauti basi nitasaini moja ya timu ya hapa ndani ambazo zinanihitaji,” anasema.
Miongoni mwa timu zinazomuhitaji ni Alliance ya Mwanza, JKT Tanzania na Tanzania Prison zote zimeelezwa kufanya mazungumzo na winga huyo aliyesajiliwa Yanga mwaka 2015 akitokea Kimondo ya Mbeya.