Luka Doncic ampoteza vibaya LeBron kwa triple-double NBA

Muktasari:

Nyota Doncic anaendelea kufanya mambo makubwa tofauti na matarajio ya wengi akipita njia za LeBron James na Michael Jordan.

Dodoma. Baada ya Supastaa wa ligi ya kikapu Marekani (NBA), LeBron James kufunga triple-double ya tisa msimu huu, mpinzani wake Luka Doncic amejibu mapigo kwa kufunga kwa mara 11 asubuhi leo.

Pointi 38, ribaundi 11 na asisti 10 alizoifungia Luka kwa timu yake Dallas Mavericks katika ushindi wa pointi 118-110 dhidi ya Chicago Bulls amethibisha ubora wake kwa kufunga triple-double mbele ya LeBron.

Luka Doncic ni nyota wa zamani wa timu ya kikapu ya Real Madrid, ameendelea kuthibitisha kwamba wachezaji kutokea barani Ulaya wanaweza kufanya kweli kwenye ligi hiyo.

Triple-double ya leo inamfanya Luka aendelee kuwa kileleni kwenye idadi nyingi zaidi za triple-double msimu huu akiwa amefikisha 11 akimuacha LeBron mwenye tisa.

Mchuano wao mkali unazidisha upinzani baina yao hata kwenye kura za kukamatia unahodha wa ukanda wa Magharibi dhidi ya ukanda wa Mashariki kuelekea mchezo wa NBA all-star.

Mchezaji atakayeongoza kwa kura ndiye atakuwa nahodha atakuwa na kazi ya kuiongoza timu yake dhidi ya mashariki inayoongozwa na nyota Giannis Antetokounmpo.