VIDEO: Katwila atoboa siri ya Mtibwa Sugar kuifunga Simba SC Mapinduzi Cup

Muktasari:

Simba ilikuwa bora kuanzia mwanzo mpaka mwisho hali hiyo ilimfanya awe makini kuzuia mbinu za wapinzani wake.

Dar es Salaam.Kocha mkuu wa Mtibwa Sugar, Zuberi Katwila amesema siri kubwa ya klabu yake kuibuka na ushindi 1-0 dhidi ya Simba katika fainali ya Mapinduzi Cup ilitokana na kuwaheshimu wapinzani wake kutokana na ubora wao.

Katwila alisema alitambua Simba itakuwa bora kuanzia mwanzo mpaka mwisho hali hiyo ilimfanya awe makini kuzuia mbinu za wapinzani wake.

"Simba ni timu bora kwahiyo nilicheza na timu bora ambayo walikuwa vizuri mwanzo mpaka mwisho, mimi nilikuwa nalinda mbinu zao kwa sababu nilikuwa najua muda wowote wanafunga," alisema.

Katwila alisema kuchukua ubingwa anaona ni faraja kubwa kwani wamekuwa wakiingia mara kwa mara, lakini wanashindwa kuchukua.

"Kiukweli huu unakuwa ni ubingwa wa pili kwetu sasa baada ya kuchukua 2010, tumeingia mara nyingi lakini hatukuweza kuchukua," alisema.

Kocha huyo alisema vijana wake walipambana katika mchezo huo bila kuahidiwa chochote kile.

"Hakuna ambacho tumeahidiwa sisi, lakini wachezaji wenyewe tu waliweka nia ya kushinda mchezo huu kwasababu ni mara yao ya kwanza wengi kicheza fainali na hicho ndio kimewapa moyo," alisema.