Aunt Ezekiel atoboa siri ya Wema kuachwa miaka kumi ya Diamond

Muktasari:

Huwezi kufanya kila jambo wanalolitaka watu, hata kama kweli mashabiki wanaona Wema alikuwa na mchango kwenye muziki wa Diamond, lakini mwenyewe ndio hivyo kaamua huwezi kumlazimisha

Morogoro.Mcheza filamu, Aunt Ezekiel ametoboa siri ya kukosekana kwa mrembo Wema Sepetu katika safari ya miaka kumi ya Diamond mkoani Kigoma.

Safari hiyo ya Diamond imeanza leo Jumamosi, Desemba, 28 2019 ambapo ameongozana na mashabiki zake na watu wake wa karibu huku wakitarajia kufika kesho Desemba 29, Jumapili jioni.

Pamoja na kuwepo kwa wasanii wengi waliochangia katika maendeleo ya Diamond kimuziki, lakini kukosekana kwa Wema kumezua gumzo mitandaoni.

Mashabiki wanakuja na kauli hiyo kutokana na mrembo huyo kuwahi kuwa katika mahusiano na Diamond wakati akiwa anaanza muziki.

Kutokana na matakwa hayo ya mashabiki, Mwanaspoti ilimuuliza Aunt Ezekiel ambaye ni rafiki wa karibu na Wema kutaka kujua kulikoni amekosekana katika safari hiyo.

Aunt amesema suala la Diamond kumualika Wema au kutomualika ni uamuzi wake mwenyewe na hakuna anayeweza kumlazimisha.

"Huwezi kufanya kila jambo wanalolitaka watu, hata kama kweli mashabiki wanaona Wema alikuwa na mchango kwenye muziki wa Diamond, lakini mwenyewe ndio hivyo kaamua huwezi kumlazimisha," amesema Aunt.

Hata hivyo alipoulizwa kama kuna ushauri wowote huwa anampa Diamond kuhusiana na Wema, Aunt amesema hawajawahi kukaa na kumzungumzia mremno huyo, kwa kuwa walishaachana na kila mtu ana maisha yake kwa sasa.

"Naanzaje kumzungumzia Wema kwa Diamond wakati najua ana mwanamke wake kwa sasa ambaye watu wote wanamjua, nadhani sipaswi kufanya hivyo kwa kuwa kila mtu ana maisha yake kwa sasa hivyo  nikifika kwa Diamond nitazungumza yanayotuhusu sisi, vilevile nitafanya hivyo kwa Wema," amesema Aunt.

Katika safari hiyo mbali na mashabiki zake, Diamond ameongozana na familia yake akiwemo mzazi mwenzake Tanasha Donna na mtoto wao, dada zake Esma Platnumz na Queen Darleen.