Straika Pamba astukia jambo FDL awatonya nyota wenzake

Muktasari:

Kundi B karibia timu tano ziko katika janga la kushuka daraja wamepishana nao pointi kati ya mbili hadi nne.

Mwanza. Mshambuliaji wa Pamba FC, Brian Hizza ameangalia msimamo wa Ligi Daraja la Kwanza katika Kundi B na kugundua nao wako katika nafasi mbaya ya kushuka msimu ujao hivyo wanatakiwa kukomaa.

Hiza alisema mpaka sasa wana pointi 22, lakini licha ya kuwepo nafasi ya nane bado wako katika janga la kushuka daraja kutokana na kupishana alama chache na timu zilizo chini yao.

Alisema wamepishana pointi nne na Green Warriors ambao wanaburuza mkiani katika Kundi B wakiwa na alama 18 kitu ambacho wanatakiwa wao kupambana kuhakikisha mechi hizo nne wanapata ushindi.

“Tuko nafasi ya nane ukiangalia katika msimamo wa ligi unaona tumepishana pointi mbili hadi nne hivyo hata sisi tuko katika janga hili la kushuka daraja msimu ujao,” alisema Hiza.

Aliwataka wachezaji wenzake kujua nao wako katika timu ambazo zinaweza kushuka msimu ujao hivyo uko walipo wanatakiwa kuendelea kujifua vilivyo ili wakirejea wawe fiti.

Hiza alisema msimu huu malengo yao kama wachezaji hayajatimia kutokana na kushindwa kuipandisha daraja timu hiyo msimu ujao hivyo sasa kilichobaki ni kumaliza mechi hizo kwa ushindi ambapo kutawafanya wabaki kwenye ligi hiyo.