Matawi Yanga yamtaka Dk Msolwa achukua hatua kwa waliomkorofisha GSM

Muktasari:

Machi 24 mwaka huu GSM aliuandikia uongozi wa Yanga barua ya kujitoa kusaidia baadhi ya mambo ndani ya klabu hiyo kutokana na viongozi wateule kutokubaliana na sapoti ambayo wanaitoa nje ya mkataba

Dar es Salaam.Matawi ya Yanga jijini Dar es Salaam yamemtaka mwenyekiti wao Dk Mshindo Msolwa kuhakikisha anawachukulia hatua viongozi wa kamati ya utendaji walimfanya GSM ajivue gamba.

Machi 24 mwaka huu GSM aliuandikia uongozi wa Yanga barua ya kujitoa kusaidia baadhi ya mambo ndani ya klabu hiyo kutokana na viongozi wateule kutokubaliana na sapoti ambayo wanaitoa nje ya mkataba.

Mratibu wa matawi ya klabu hiyo, Kais Edwine alisema wao wapo pamoja na GSM hivyo DK Msolwa awachukulie hatua wahusika haraka iwezakanavyo.

Kais alisema matawi hayatakubali kuona mtu au kundi la watu wanamuhujumu GSM kwa maslahi yao binafsi.

"Hao viongozi waliofanya hivyo kama wao wanaona namna gani waondoke Yanga ila wamuache GSM anayejitolea kwa mapenzi ya dhati,"

Aidha wamemtaka Dk Msolwa asipochukua hatua basi wao watashinikiza mkutano wa dharura ili wakafanye uamuzi ya kuwaondoa.

Viongozi hao wa matawi waliudhuria kwa uchache klabu hapo kutokana na kuepuka mkusanyiko kutokana na gonjwa la corona.