Harmonize: Albumu yangu itawafariji katika kipindi hiki cha corona

Muktasari:

Harmonize amesema ni muda wa kutulia na familia nyumbani na kupata nafasi ya kusikiliza nyimbo nzuri za albamu yake mpya zitawafariji.

Dar es Salaam.Mwanamuziki, Harmonize 'Konde Boy' amewataka Watanzania kuchukulia kwa uzito suala la kujitenga na kuacha mikusanyiko isiyokuwa ya lazima ili kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa corona.

Harmonize amesema ni muda wa kutulia na familia nyumbani na kupata nafasi ya kusikiliza nyimbo nzuri za albamu yake mpya zitawafariji.

Konde Boy amesema utii ni bora kuliko shuruti akimanisha kukwepa mikusanyiko ni kinga kuliko kukusanyika kisha watu wakaanza kuhangaika kujitibia.

"Ni Jambo la usikivu ambalo ni faida kwa afya zetu, kwa hiyo tuunge mkono juhudi za serikali ili janga hili lipite tuweze kurejea katika kazi zetu."

"Katika albamu yangu mpya kuna nyimbo za faraja ambazo ukikaa na mpenzi wako iwe nyumbani ama ufukweni basi utasikia raha."

Harmonize amesema anaamini Watanzania wasikivu wa kupambana na kupunguza ama kutoeneza maambukizi ya corona kwa kukaa majumbani mpaka watakaposikia amri ya serikali.