Mtibwa wala haina mpango

Muktasari:

  • Hatuna ulazima wa kufanya usajili dirisha dogo kikosi chetu kimejikamilisha kinaweza kufanya kazi katika mazingira yote hivyo kushiriki kwetu kombe la Shirikisho hakuwezi kutufanya tukaanza upya kufanya usajili wakati wachezaji wapambanaji wapo.

DIRISHA dogo la usajili linakaribia kufunguliwa mwezi ujao, lakini benchi la ufundi la Mtibwa Sugar, limefichua wala halina mpango wa kuongeza mtu kikosini kwa vile mziki wao umekamilia vya kutosha.

Kocha Mkuu wa timu hiyo, Zuberi Katwila alisema hana sababu ya kuongeza mchezaji katika dirisha hilo labda kama itatokea tatizo kubwa kwa mchezaji wao muhimu.

Alisema kikosi chake kipo kamili na kina wachezaji wenye uwezo wa kufanya vizuri na kuisaidia timu katika mashindano yote yaliyo mbele yao, hivyo wanachofanya sasa ni kuboresha kuwaongezea mikataba waliopo wasiondoke.

Kuhusu kipigo cha bao 1-0 walichopewa na Mbao, alisema vijana wake walizidiwa ujanja, japo walipambana kusaka matokeo mazuri. Mtibwa ilifungwa ugenini Uwanja wa CCM Kirumba na kuendeleza rekodi yao ya unyonge mbele ya timu hiyo.