Mkwasa apewa siri ya Molinga kutupia

Muktasari:

Akizungumzia spidi yake ya kutupia wavuni ambayo mpaka hivi sasa mshambuliaji huyo ana mabao manne, Zahera alisema Molinga atafunga sana kwenye ligi.

KOCHA Mwinyi Zahera aliyekuwa anaifundisha Yanga amemtonya kocha wa muda wa kikosi hicho, Charles Mkwasa kwamba kama anataka mshambuliaji wake David Molinga ‘Falcao’ awe anafunga mara kwa mara amchezeshe akiwa mshambuliaji wa mwisho.

Zahera alisema mshambuliaji huyo anakuwa mzuri pale anapokuwa anasubiri kupewa mipira na wenzake na yeye kutupia tu wavuni huku akisisitiza kuwa eneo hilo lazima afanye vizuri.

“Falcao sio mchezaji ambaye anaweza kupambana sana akitokea nje, kama ambavyo wanafanya Kagere au Makambo lakini yeye akiwa ndani ya boksi akipokea mpira ni ngumu mno kukukosa,” alisema.

Zahera aliliambia Mwanaspoti kwamba mchezaji huyo katika mipira 15 ana uwezo wa kuingiza wavuni hata 10 na anaamini katika uwezo mkubwa alionao.

Akizungumzia spidi yake ya kutupia wavuni ambayo mpaka hivi sasa mshambuliaji huyo ana mabao manne, Zahera alisema Molinga atafunga sana kwenye ligi.

Alisema mchezaji huyo kwa namna ambavyo anafunga anaweza kufunga magoli 20 na si 15 kama ambavyo alisema awali.

“Falcao amefunga magoli mengi, lakini yamekuwa yakikataliwa kila mara, kama yangekubaliwa angekuwa mbali lakini hilo naamini atafunga mengi zaidi,” alisema.

Zahera ndiye aliyemsajili nyota huyo na kumvumilia licha ya kwamba alikuwa akibezwa mwanzoni alipokuwa anashindwa kufunga.

Mchezaji huyo alisajiliwa Yanga katika dakika za lalasalama za kipindi cha usajili mkubwa.