Mchezaji wa pili Liverpool akutwa na corona

Muktasari:

Liverpool imethibitisha nyota wake Sadio Mane kuwa na maambukizi ya corona, mchezaji huyo ni wa pili kwa timu hiyo kukutwa na maambukizi hayo.

LONDON, ENGLAND. SIKU tatu baada ya Thiago Alcantara kutangazwa kukutwa na maambukizi ya ugonjwa wa corona, Sadio Mane amekuwa mchezaji wa pili wa Liverpool kukutwa ugonjwa huo.

Liverpool wamesema winga huyo wa Senegal amekutwa na dalili za ugonjwa huo lakini hata hivyo hali yake ya kiafya inaendelea vizuri.

Mane, 28, alikuwa sehemu ya kikosi cha Liverpool ambacho kiliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Arsenal kwenye mchezo uliopita wa Ligi Kuu England.

Winga huyo, aliukosa mchezo wa kombe la Carabao dhidi ya Arsenal ambao walicheza nao kwenye Ligi kutokana na dalili alizokutwa nazo za virusi vya corona hivyo kwa sasa amejiweka karantini.

Taarifa rasmi iliyotolewa na Liverpool, inasema, "Kama ilivyokuwa kwa Thiago Alcantara, Liverpool imeendelea kufuata taratibu zote zinazohusiana na mtu mwenye corona, Mane amejitenga kwa muda unaotakiwa kitaalamu"

Mane,ambaye amefunga mabao matatu kwa Liverpool msimu huu yote kwenye Uwanja wa Anfield, ataukosa mchezo ujao dhidi ya Aston Villa, Jumapili kabla ya mapumziko ya wiki ya kimataifa.

Jumatatu, walitangawa watu 10 katika Ligi Kuu England kukutwa na virusi vya corona, ilikuwa idadi kubwa zaidi ya maambukizi  kutokea tangu msimu huu kuanza.