Mateo ashangaa Ligi ya Zanzibar kutoanza mpaka sasa
Straika wa KMKM, Matheo Antony amesema soka la Zanzibar, linachukua muda mrefu mpaka mchezaji kufanikiwa kucheza nje ya nchi tofauti na a Bara kwa sababu linafuatiliwa zaidi na nchi mbalimbali.
Mateo alisema soka la Zanzibar ni changamoto kwani mpaka sasa hawajui ligi ya huko inaanza lini, kitu anachoona kinawashusha ari yakupambana, kutokana na kusubiria muda mrefu, wakati wenzao wa Bara wakiendelea na kazi.
"Bara wanaendelea na ligi, wakati sisi hatujui ni lini tunaanza kitu ambacho kinafanya wakati mwingine ushindani unakuwa mdogo, lakini tunapaswa kupambana hivyo hivyo kwa kadri tunavyoweza ili kufanikisha ndoto zetu,"
"Ni rahisi mchezaji wa Bara kufanikiwa kwa uharaka kwasababu, ligi ya huko ina wafuasi wengi.Nazungumzia , hilo kwasababu nimecheza Yanga na Polisi Tanzania nimeona hilo,"amesema Matheo.
Mchezaji huyo ambaye amesaini mkataba mfupi na KMKM, mbali nakuzungumzia jinsi soka la Zanzibar kuwa na changamoto pia amesema Yanga ina kikosi kizuri msimu huu hivyo anaamini wanaweza kuchukua ubingwa.
"Tumecheza na Yanga mechi ya kirafiki ambayo ni timu yangu ya zamani, safari hii imejitahidi kusajili kwani nimemuona kiungo Mukoko Tunombe, jamaa ni hatari, naamini akilizoea soka la Tanzania anaweza akafanya kitu kikubwa chakuisaidia timu yake,"alisema.