Matasi: Sitishiki na Samatta, Mane wala Mahrez

Muktasari:

  • Safu ya ushambuliaji ya Tanzania itaongozwa na Mbwana Samatta, Senegal Sadio Mane na Algeria Riyadh Mahrez.

Nairobi. Kipa namba moja wa Harambee Stars na Klabu ya St. Georges ya Ethiopia, Patrick Matasi amesema hatishwi na wachezaji wenye majina makubwa kwenye timu pinzani.

Matasi alisema kuwa anatambua kuwa Tanzania iko na mkali wa mabao katika Ligi Kuu Ubelgiji, Senegal inaye kinara wa mabao wa EPL na mshindi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, na mshindi wa taji la EPL, lakini hilo wala halimnyimi usingizi.

"Najua timu zingine kwenye kundi letu ni wakali, lakini hilo wala halininyimi usingizi, tuko tayari kwa mapambano, tutawaonesha kuwa na sisi tumejipanga kisawasawa," alisema Matasi.

Kenya inayoshiriki fainali hizi kwa mara ya kwanza baada ya kuzikosa kwa miaka 15, imepangwa kundi C, pamoja na Tanzania, Senegal na Algeria. Safu ya ushambuliaji ya Tanzania itaongozwa na Mbwana Samatta, Senegal Sadio Mane na Algeria Riyadh Mahrez.

Kikosi cha Migne, kitacheza mechi mbili za kirafiki ya kwanza, ikipigwa kesho (Juni 7), Jijini Paris dhidi ya Madagascar na ya pili ikiwa ni dhidi ya DR Congo, itakayopigwa Juni 15, Jijini Madrid.

Stars, itaanza kutupa karata yake Juni 23, dhidi ya Algeria, kisha itavaana na Tanzania (Juni 27) kabla ya kumalizana na Senegal, Julai mosi. Mechi zote zitapigwa Cairo, katika uwanja wa Juni 30.

Kikosi cha Stars:

Makipa: Patrick Matasi, John Oyemba, Faruk Shikalo

Mabeki: Abud Omar, Joash Onyango, Joseph Okumu, Musa Mohammed, David Owino, Bernard Ochieng, Brian Mandela, Philemon Otieno, Eric Ouma

Viungo: Victor Wanyama, Anthony Akumu, Ismael Gonzalez, Ayub Timbe, Francis Kahata, Ovella Ochieng, Dennis Odhiambo, Eric Johanna, Paul Were, Cliffton Miheso, Johanna Omollo

Mastraika: John Avire, Masud Juma, Christopher Mbamba, Michael Olunga