Man United yakubaliwa dau la Maguire

Muktasari:

Awali Man United na wapinzani wao wa jiji moja, Man City walishindana kumnasa beki huyo. City ilisema isingeweza kutoa zaidi ya Pauni 70 milioni.

GAZETI la The Sun la Uingereza limeripotiwa kudai kwamba Manchester United imeingia makubaliano na Leicester City kulipa kiasi cha Pauni 80 milioni kwa ajili ya kumchukua beki wa kati, Harry Maguire na jana Jumatatu staa huyo alitazamiwa kupimwa afya jijini Manchester.

Dau hilo litamfanya Maguire awe beki ghali zaidi wa soka kwa sasa na hivyo kumpiku beki wa kimataifa wa Uholanzi, Virgil van Dijk ambaye Liverpool ililipa dau la Pauni 75 milioni katika dirisha la Januari mwaka jana kupata huduma zake kutoka Southampton.

Manchester United italipa kwanza dau la Pauni 60 milioni kwa ajili ya beki huyo wa kimataifa wa England na baadaye itamalizia Pauni 20 milioni kutokana na jinsi staa huyo atakavyoendeleza kiwango chake akiwa Old Trafford.

Awali Man United na wapinzani wao wa jiji moja, Man City walishindana kumnasa beki huyo. City ilisema isingeweza kutoa zaidi ya Pauni 70 milioni.